Tuesday, April 26, 2016

Sheria ya kumlinda mtoto imeshindwa kuzuia ajira kwa watoto?



  Na Albano Midelo

Utumikishaji watoto wadogo bado unaendelea nchini Tanzania licha ya serikali kuweka sheria ya kumlinda mtoto mwenye umri usiozidi miaka 18.


Nimepita katika baadhi ya maeneo mjini Songea na kubaini idadi kubwa ya watoto wenye umri kati ya miaka tisa na 12 ambao wanazunguka kuuza bidhaa ndogo ndogo na wengine wanaombaomba.

Said Ally ni mtoto anayesoma darasa la pili katika shule moja mjini Songea ambaye anafanya biashara ya kuuza karanga za kukaanga.

“Nimeanza biashara hii tangu darasa la kwanza  nikitoka shuleni saa tano nafika mjini kuuza karanga katika maeneo mbalimbali yakiwemo ya klabu za pombe,
hadi kufika saa tisa nakuwa nimemaliza kuuza karanga ambapo kwa siku Napata shilingi 5000’’,anasema.

Anadai pesa anayopata inamsaidia yeye na familia yake kuendesha maisha kila siku,ingawa amekiri kuwa inamwathiri katika masomo yake kwa kuwa hapati muda wa kutosha kushiriki katika masomo.

Uchunguzi ambao nimeufanya katika viunga mbalimbali vya mjini Songea majira ya usiku wa kuanzia saa mbili hadi saa tano usiku nimeshuhudia makundi ya watoto wadogo wakifanyabiashara hatarishi kutokana na mazingira.

Tatizo la kuwatumikisha watoto wadogo kazi halifanyiki  kwa ajili ya biashara pekee  bali pia watoto wameonekana  wakifanyishwa kazi katika maeneo mengine kama vile maeneo ya machimbo,kazi za ndani na uvuvi.

Kwa mfano katika machimbo ya Tanzanite Mirereni mkoani Manyara watoto wadogo wanatumikishwa  kuingia katika mashimo madogo yenye kipenyo kidogo kwenda chini ardhini kwa kutumia ngazi au kamba jambo ambalo ni hatari kwa watoto kiafya.

Mwambao mwa ziwa Nyasa mkoani Ruvuma kuna idadi kubwa ya watoto ambao wameacha shule na kufanyakazi ya uvuvi wa samaki licha ya kulipwa ujira mdogo.

Sheria ya haki za mtoto ya mwaka 2009 inabainisha wazi kuwa mtu hataruhusiwa kumuajiri au kumshughulisha mtoto katika aina yoyote ya kazi itakayomnyonya mtoto.



Kwa mujibu wa sheria hiyo,mtoto ana haki ya kulindwa dhidi ya kutengwa au matendo yoyote yanayoweza kuwa na athari mbaya kwake kwa kuzingatia umri na uwezo wake.



Sheria inabainisha kuwa,kazi itakuwa ni ya kinyonyaji kwa mtoto iwapo inamnyima mtoto kuwa na afya njema au maendeleo,haifai kwa umri wake au mtoto hapati malipo ya kutosha.



Mtu yeyote anayevunja sheria katika kifungu hicho,sheria inaelekeza wazi kuwa atakuwa anatenda kosa na akitiwa hatiani atawajibika kulipa faini isiyopungua shilingi laki moja au kutumikia kifungo kwa muda wa miezi mitatu au vyote kwa pamoja.

Tanzania ni miongoni mwa nchi 174 zilizoridhia Azimio la umoja wa mataifa namba 182 la kukomesha utumikishaji watoto chini ya umri wa miaka 18.

Hata hivyo uchunguzi umebaini kuwa pamoja na jitihada za serikali za kupiga vita utumikishaji watoto bado watoto wamekuwa wakitumikishwa katika maeneo mbalimbali nchini kwa visingizio mbalimbali ambavyo havina msingi wowote.

Shirika la Kuteteta Haki za Binadamu la Human Rights Watch limetangaza kuwa, watoto wa maeneo ya migodi nchini Tanzania wanakabiliwa na  mazingira magumu.

Ripoti inabainisha inataja idadi kubwa ya watoto wameathirika kiafya kutokana na kufanyishwa kazi ngumu zikiwemo za kwenye migodi.

Kulingana na  ripoti  hiyo,kuna vitendo vya dhuluma na ukatili wa kingono unaofanywa dhidi ya watoto hao na kwamba watoto wapo katika hatari ya kupata magonjwa mbalimbali kutokana na vumbi la madini.

Umoja wa Mataifa ulipitisha mkataba wa haki za watoto ili kumlinda mtoto asinyanyaswe na kukoseshwa haki zake za msingi kama vile kupata elimu, matunzo na kadhalika.

Ajira ya watoto ni tatizo sugu ambalo halijapatiwa ufumbuzi katika nchi nyingi zinazoendelea ikiwemo Tanzania,huku sababu kubwa ikitajwa kuwa ni ujinga,maradhi,vita na umaskini.

Kupitia katika vyombo mbalimbali vya habari tumeshuhudia watoto wakilazimika kufanya kazi ngumu ya kuponda kokoto ili kuweza kupata fedha za kuendeshea maisha ya familia hivyo kuathiri taaluma.

Ruvuma,Mwanza,Arusha,Mbeya,Dar es salaam na Morogoro ni miongoni mwa mikoa ya Tanzania yenye idadi kubwa ya watoto walioacha shule na kugeuka kuwa watoto wanaofanya biashara ndogondogo na wengine wamegeuka ombaomba.


Ukitembea katika miji hiyo ni jambo la kawaida kukutana na watoto ambao walitakiwa kuwa shuleni  badala yake wamekuwa watoro,wakifanya biashara ndogondogo ili waweze kujikomboa kiuchumi.


Utafiti umebaini kuwa baadhi ya watoto hulala katika veranda za maduka makubwa yaliyopo katika miji na wengine hulala katika maeneo ya vituo vya mabasi.

Rais mstaafu Jakaya Kikwete mwaka 2014 alishtushwa na kiwango kikubwa cha wanafunzi wa shule za msingi katika mkoa wa Ruvuma kushindwa kuhudhuria na kumaliza shule kwa sababu mbalimbali, ukiwemo utoro.

Changamoto ya utoro  ni kubwa hapa nchini kwa mfano katika mkoa wa Ruvuma,takwimu za utoro zinaonesha kuwa kati ya watoto 41,801 walioanza shule ya msingi mwaka 2007 ni watoto 30,698 waliofanya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka 2013.

Takwimu za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi zinaonesha kuwa, tangu mwaka 2004 hadi 2008, wanafunzi wa kike 28,600 walishindwa kuendelea na masomo huku sababu nyinginezo ikiwa ni utoro,ajira na mimba za utotoni.


Kuendelea kuwepo watoto  wanaoacha masomo kutokana na sababu mbalimbali, kunaipa serikali changamoto kubwa ikizingatiwa wadau wa elimu wamekuwa wakifuatilia kwa karibu kuhimiza usawa wa kijinsia katika elimu.


Tathmini ya ripoti ya malengo ya maendeleo ya milenia (MDGs) inaonesha kwamba serikali ilidhamiria kuhakikisha ifikapo mwaka huu 2015, hakuna mwanafunzi wa shule ya msingi anayekatiza masomo,jambo ambalo limeshindikana kwa sababu idadi ya watoto wanaoacha shule kwa sababu mbalimbali inaongezeka badala ya kupungua.



No comments:

Post a Comment