Ama kweli hujafa hujaumbika
Na Kwirinus Mapunda
“Nisingekatwa miguu
yote miwili ningekufa siku nyingi kwa kuwa madaktari walisema mifupa ya miguu
yote imeathirika dawa pekee ni kukatwa miguu yote ili niweze kuendelea
kuishi’’,anasema Beatrice Ndomba kwa masikitiko makubwa.
![]() |
| Beatrice baada ya kukatwa miguu |
Mtawa anayefahamika kwa
jina moja la Sr.Lucy kutoka shirika la
watawa wa mtakatifu Vincent jimbo katoliki la Mbinga ambaye anahusika na idara
ya wenye ulemavu wa viungo ndiye aliyemchunguza na kubaini miguu yake
imeathirika ndipo alimfadhili nauli na fedha za matibabu katika hospitali ya
Ikonda wilayani Makete mkoani Njombe.
“Baada ya kufika katika
hospitali hiyo nilipigwa X RAY,na kubaini kuwa wadudu wa hatari walikuwa
wameshaingia hadi katika mifupa,madaktari walinishauri kuwa iwapo mguu huo
hautakatwa wadudu hao wataathiri katika maeneo muhimu hadi kwenye moyo na kunisababishia kifo
hivyo nilikubali kukatwa mguu wangu wa pili
hivyo kubakia bila miguu lakini
nikiwa mzima wa afya’’,alisema.
Hata hivyo anasema
tangu amekatwa mguu wa pili maumivu yote yamekwisha isipokuwa sasa amekuwa
tayari mlemavu wa viungo na kwamba anamshukuru Sr.Lucy kwa utaalamu wake pamoja
na kumpatia misaada mbalimbali ya fedha na baiskeli ya wenye ulemavu ambayo
anaitumia hivi sasa.
Beatrice
anahitaji msaada wa miguu ya bandia hivyo mfadhili yeyote ambaye anaweza kumsaidia
gharama za viungo hivyo bandia atakuwa ametoa mchango mkubwa kwa Beatrice.
Beatrice mwenye umri wa
miaka 23 alizaliwa mwaka 1992 ,hivi sasa ni mlemavu wa viungo baada ya kukatwa
miguu yake yote miwili,anaishi katika mtaa wa Ruhuwiko kanisani manispaa ya
Songea mkoani Ruvuma anapatikana kwa namba ya simu 0766642634 au 0673054535 unaweza kuwasiliana naye.
Anabainisha kuwa mguu
wake wa kwanza alikatwa mwezi Agosti,2012
katika hospitali ya Rufaa ya Peramiho iliyopo kilometa 24 kutoka mjini Songea na mguu wake wa pili alikatwa Julai 2014 katika hospitali ya Ikonda
wilayani Makete mkoani Njombe.
Anasema alizaliwa
salama kabisa wala hakutarajia kwamba siku moja atakuwa mlemavu,amesoma darasa
la kwanza shule ya msingi Ruhuwiko manispaa ya Songea,kisha kuendelea na darasa
la pili hadi la saba jijini Mbeya ambako alikuwa anaishi na wazazi wake.
Alijiunga na elimu ya sekondari ya Forest iliyopo
jijini Mbeya ambako alisoma kuanzia kidato cha kwanza hadi kufanikiwa kumaliza
kidato cha nne mwaka 2010 akiwa hana
ulemavu wowote.
Hata hivyo anasema
mwaka 2012 tatizo lililosababisha kupata ulemavu wa viungo lilianza akiwa
amejiunga kwa ajili ya masomo stashada ya uhasibu katika chuo cha Uhasibu jijini
Mbeya mwaka wa kwanza ndipo alianza kupata maumivu makali katika mguu wake
mmoja hali iliyomsababishia kushindwa kuendelea na masomo na kurudi Songea kwa
ajili ya matibabu zaidi.
“Homa ilianza kwa kujisikia
kama dalili za ugonjwa wa malaria hivyo nilipewa dawa aina ya SP ambayo
haikuweza kunisaidia ndipo nilipelekwa hospitali ya Songea ambapo nilitundikiwa
dripu la kwinini ambayo pia haikusaidia, homa iliendelea kwa kasi huku nikipata
maumivu makali kwenye miguu ambayo
ilikuwa kama inawaka moto’’,alisema.
Kutokana na kutopata
nafuu siku iliyofuata asubuhi alipelekwa
katika hospitali ya Rufaa ya misheni Peramiho ambapo madaktari walijitahidi
kumuhudumia.
![]() |
| Beatrice kabla hajakatwa miguu |
Hata hivyo anasema
maumivu ya miguu yaliendelea huku miguu ikianza kuvimba na kuwa na rangi nyeusi
na kutoa malengelenge ambayo yanafanana na mtu aliyeungua moto ambapo madaktari
walishauriana na kuamua kuichubua ngozi na kutibu kama vidonda.
Uchunguzi zaidi
uliofanywa na madaktari wa hospitali ya Peramiho
ulibaini kuwa mguu mmoja uliharibika kabisa hivyo waliamua kuukata jirani ya
goti hali iliyomsababishia kupata ulemavu kwa kubakiwa na mguu moja ambao bado
ulikuwa na kidonda ambacho kiliendelea kumsumbua.
Beatrice anadai kuwa madaktari
hao walimweleza chanzo cha tatizo la miguu yake kuathirika lilitokana na athari
za dawa ya SP na dripu la kwanini ambayo alikunywa na kutundukiwa kwa lengo la
kutibu ugonjwa wa malaria.
Anasema kidonda ambacho
kilikuwepo katika mguu mmoja kiliendelea kumsumbua kuanzia mwaka 2012 hadi 2014
na kumsababishia gharama kubwa ya nauli na matibabu ya kwenda Peramiho kila baada
ya siku moja madaktari walimtaka
kufungia kidonda.
Kutokana na kushindwa
kumudu gharama ndipo bibi yake aliamua kwenda kuomba msaada kwa mhasibu wa
nyumba ya watawa wa kanisa katoliki wa Vincent Ruhuwiko mjini Songea Sr.Lea
Haule ambaye alimsaidia nauli ya watu wawili na gharama za kufungia kidonda
kila baada ya siku moja.
Hata hivyo Sr.Lea
alimtafuta Sr Lucy ambaye anahusika na kitengo cha walemavu wa viungo mjini
Mbinga mkoani Ruvuma ili aone uwezekano wa kumtengenezea mguu wa bandia
Beatrice .
Hata hivyo Sr.Lucy
mtaalam wa watu wenye ulemavu wa viungo alipomchunguzwa kwa makini alibaini kuwa kumtengenezea mguu
wa bandia bado haitasaidia kwa kuwa mguu wake mmoja aliubaini una matatizo
makubwa ambayo yanatakiwa kwanza kufanyiwa uchunguzi wa kudumu katika hospitali nyingine.
Hatimaye Sr.Lucy mwezi
Julai 2014 alimsaidia Beatrice na mtu wa kumuuguza nauli na fedha za matibabu
na matumizi kwenda katika hospitali ya misheni ya Ikonda wilayani Makete mkoani
Njombe ambayo inatajwa kuwa na madaktari bingwa wa matatizo ya viungo vya
binadamu ambako aliweza kutibiwa baada ya kukatwa mguu wake wa pili.
Hata hivyo anasema
ndoto zake za kusomea uhasibu zimeyeyuka kwa kuwa kutokana na ulemavu alionao
hawezi tena kuwa mhasibu badala yake hivi sasa anapenda kujifunza lugha ya kiingereza ,kusomea kompyuta pamoja na
kujifunza ufundi wa kushona nguo na kudalizi vitambaa.
“Ndoto zangu hivi sasa
ni kufungua kiwanda cha ushonaji kwa kuanzia nikipata mashine mbili za kushonea
nitaweza kujitegemea mwenyewe,nawaomba watanzania wanaoweza kunisaidia mashine
hizo pamoja na misaada mingine nitashukuru kwa kuwa mimi tayari ni mlemavu
nikiwezeshwa naweza’’,alisisitiza.
Beatrice ambaye ni
yatima ndiye mtoto wa kwanza kuzaliwa
katika familia ya watoto tisa
anahitaji msaada wa hali na mali katika kipindi hiki ambacho hana ajira
zaidi ya kutegemea misaada ya wahisani mbalimbali.
Hata hivyo anasema yeye
pamoja na wadogo zake hawana sehemu
maalum ya kuishi,kwa sababu wamefadhiliwa katika nyumba moja katika eneo la
Ruhuwiko na kwamba anatamani kuishi na kujitegemea ili aweze kuwalea wadogo
zake ambao wanamtegemea.
Watu
wenye ulemavu kama sehemu ya jamii ya Tanzania,ni watu muhimu na wanastahili
kupata haki zao kama watu wengine wasiokuwa na ulemavu.
Kwa
kutambua umuhimu huo, Bunge la Jamhuri wa Muungano wa Tanzania lilipitisha
rasmi Sheria namba 9 ya Watu Wenye Ulemavu ya mwaka 2010. Adhima kuu ya sheria
hii ni kutoa haki na fursa mbalimbali kwa watu wenye ulemavu. Pia inakataza
aina zote za ubaguzi dhidi yao.
Kwa
mujibu wa sheria hiyo mwenye ulemavu ana Haki ya kutambuliwa na kuheshimiwa,
Haki ya kuwezeshwa na kuwekewa
miundombinu ya kuyafikia na kuyatumia majengo ya umma,Haki ya kupata nyenzo za
kujimudu mfano, fimbo nyeupe kwa wasioona, kiti cha magurudumu matatu kwa wenye
ulemavu wa viungo na Haki ya kufanya kazi na kupata ajira.
mapundakwirinus@yahoo.com,simu 0677006096


No comments:
Post a Comment