Monday, May 9, 2016

Visiwa viwili vilivyouzwa Nyasa vimerejeshwa serikalini

Mzungu alinunua bila kufuata sheria

Na Albano Midelo

VISIWA viwili  vya Mbambabay na Lundo katika ziwa Nyasa mkoani Ruvuma ambavyo viliuzwa kinyume cha sheria kwa mwekezaji kutoka nje ya nchi kati ya mwaka 2004 na 2005 vimerejeshwa serikalini.
Kisiwa cha Lundo ambacho kiliuzwa kimerejeshwa serikalini
 Mwandishi wa makala haya mwaka 2014 na 2015 aliandika kuhusu uuzaji wa visiwa hivyo kinyume cha sheria kwenye mitandao ya kijamii pamoja na gazetini.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Nyasa Jabir Shekimweri alisema viongozi wa vijiji waliuza visiwa hivyo kwa malipo ya shilingi kati ya milioni nne hadi tano na kwamba baada ya kubaini kuwepo kwa ukiukwaji wa sheria
uongozi wa Halmashauri ulimwita mwekezaji huyo  ambaye alikiri kununua visiwa hivyo kinyume cha sheria.

Awali mwekezaji huyo akiwa na mwanasheria wake alidai kuwa amenunua visiwa hivyo kwa mikataba halali na viongozi wa vijiji hata hivyo mwishone ilibainika kuwa sheria haimruhusu mwezezaji kumilikishwa visiwa.

Afisa ardhi wa Halmashauri ya wilaya ya Nyasa Christopher Komba ambaye pia ni mwanasheria anabainisha kuwa Halmashauri ya kijiji cha Mbambabay iliuza kisiwa cha Zambia kilichopo katika kijiji hicho na Halmashauri ya kijiji cha Lundo iliuza kisiwa cha Lundo kati ya mwaka 2004 na 2005.

“Viongozi hao waliuza visiwa hivyo kwa mzungu mmoja aliyefahamika kwa jina la John Tinny ambaye alilipa kati ya shilingi milioni tano na kila mwaka alikuwa analipa kodi lakini baadaye baada ya Halmashauri ya Mbinga kugawanywa kuwa na Halmashauri ya Nyasa ndipo ufuatiliaji wa kina ulifanyika na serikali kufanikiwa kuvirejesha visiwa hivyo’’,alisisitiza Komba.
Kisiwa cha Zambia kilichopo Mbambabay ambacho kiliuzwa

Kwa mujibu wa Komba visiwa hivyo vipo katika maeneo nyeti ambayo kimsingi hairuhusiwi kumilikishwa  na kwamba visiwa vinasimamiwa na mamlaka nyingine na sio Halmashauri ya vijiji kwa mujibu wa sera ya Taifa ya ardhi ya mwaka 1995,sheria ya usimamizi wa mazingira ya mwaka 2004 pamoja na sheria ya uvuvi.

Akizungumzia kodi ambayo alikuwa anadai analipa mwekezaji huyo katika Halmashauri ya kijiji kila mwaka,Komba amebainisha kuwa mwekezaji huyo kulipa kodi hiyo alikuwa anafanya makosa kwa kuwa kodi hiyo ilitakiwa kupangwa na waziri wa ardhi na maendeleo ya makazi na sio Halmashauri ya kijiji kwa kuwa kisiwa sio sehemu ya kijiji.

Diwani wa kata ya Lipingo Cathbert Ngwata ambaye kisiwa hicho kipo katika kata yake amekiri Kisiwa maarufu kilichopo mpakani mwa vijiji vya  Lundo na Ngindo kiliuzwa kwa raia mmoja wa kigeni  kinyume cha sheria za nchi.

Michael Milinga afisa mtendaji wa kata ya Lipingo yenye vijiji vitatu ambavyo ni Ngindo,Lundo na Lipingo anasema kisiwa hicho kina maliasili za kuvutia zikiwemo wanyama,ndege,wadudu pamoja na mimea ya aina mbalimbali.

Kwa mujibu wa afisa mtendaji huyo  toka ufukweni hadi ndani ya kisiwa hicho ni mwendo wa nusu saa kwa mtumbwi na kwamba raia huyo wa kigeni ambaye aliuziwa kisiwa hicho aliwatumia viongozi wenyeji wa vijiji kuendesha mchakato mzima wa  kuuziwa kisiwa hicho.

“kuna raia mmoja wa kigeni alifika kuomba kumilikishwa kisiwa cha Lundo ili aweze kuwekeza mwanzoni makubaliano na uongozi wa kijiji ilikuwa anafanya malipo katika kijiji kwa miaka mitano na baadaye aliomba kwa miaka kumi’’,alidai Milinga.

 Uchunguzi unaonesha kuwa baadhi ya viongozi wa vijiji  waliingia mkataba wa kumuuzia raia wa kigeni kisiwa hicho bila kuwashirikisha wananchi wote licha ya kwamba kisiwa hicho sio sehemu ya kijiji kwa kuwa kipo ndani ya ziwa Nyasa.

 Hata hivyo baadhi ya wananchi wameipongeza hatua ya uongozi wa Halmashauri ya wilaya ya Nyasa kumnyang’anya visiwa hivyo mwekezaji na kwamba tangu awali walikuwa hawaungi mkono hatua ya viongozi wao wa vijiji kumuuzia mgeni kisiwa hicho kwa kuwa kina manufaa makubwa kwa wavuvi ambao wamekuwa wanakitumia kupumzika  na kujihifadhi ziwa linapokuwa na dhoroba kali.

“Iwapo raia huyo wa kigeni angemilikishwa kisiwa hicho angeweza kuweka masharti magumu yakiwemo kutoruhusu sisi wavuvi kupumzika katika eneo hilo la kisiwa hali ambayo ingehatarisha maisha yetu kwa sababu ziwa Nyasa ni moja ya maziwa yenye dhoruba kali’’,alisisitiza mvuvi John Challe. .

Kisiwa hicho kinachokadiriwa kuwa na   ekari kati ya 60 hadi 70 kinadaiwa kuanza mchakato wa kuuzwa tangu mwaka 2004  na kwamba mwekezaji  anadaiwa mara baada ya kununua kila mwezi  alikuwa analipa ushuru wa shilingi 400,000 katika kijiji cha Lundo.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Nyasa Jabir Shekimweri

Afisa maliasili wa Halmashauri ya wilaya ya Nyasa Bugingo Bugingo anasema sheria za nchi haziruhusu mtu binafsi kumilikishwa fukwe,mlima au kisiwa na kusisitiza kuwa ni kosa kubwa kummilikisha mtu binafsi na hasa raia wa kigeni eneo ambalo linatambulika kisheria kuwa ni hifadhi.

“kulingana na sheria za Tanzania kisiwa chochote kilichopo ndani ya bahari au ziwa hairuhusiwi kummilikisha mtu yeyote ispokuwa sheria inaruhusu kuwekeza’’,anasisitiza mtaalam huyo wa mazingira.

 Dk.Rugemeleza Nshala ni  mwanasheria na mkurugenzi wa chama cha wanasheria watetezi wa mazingira Tanzania (LEAT) anabainisha kuwa kisheria mtu binafsi anaruhusiwa kumiliki ardhi lakini haruhusiwi kumiliki visiwa vidogo,fukwe,vilele vya milima,kingo za mito,maeneo yote oevu au chepechepe pamoja na njia za asili za wanyamapori.

Hata hivyo amesema watu ambao tayari wametwaa fukwe na visiwa na kuwazuia watu wengine au kuwalipisha pesa wanakiuka kanuni ya msingi ya matumizi ya raslimali za pamoja na kwamba ni jukumu la  kila mwananchi kupinga kubinafsishwa kwa visiwa au fukwe ambazo ni zawadi tuliopewa na Mungu.

Mbunge wa jimbo la Nyasa Injinia Stella Manyanya ambaye pia ni Naibu waziri wa elimu,Sayansi,Teknolojia na Ufundi, ametoa wito kwa wadau wote wa sekta ya utalii  mkoa wa Ruvuma kuhakikisha kuwa wanayalinda maeneo yote yaliohifadhiwa hasa mwambao mwa ziwa Nyasa ambako kuna rasilimali muhimu zinazoweza kufungua sekta ya utalii.

 Tangu serikali ilipotangaza kufunguliwa kwa Mtwara korido pamoja na kutangazwa kwa wilaya ya  Nyasa  wawekezaji wengi wamekuwa wanajitokeza kutafuta maeneo ya uwekezaji mwambao mwa ziwa Nyasa huku baadhi yao wakipata maeneo kwa njia haramu ikiwemo   kuwatumia viongozi wa vijiji  bila kuwahusisha wananchi.

Ziwa Nyasa limezungukwa na nchi tatu ambazo ni Tanzania,Malawi na Msumbiji.Ziwa hilo lipo kwenye usawa wa meta 500 toka usawa wa bahari kina cha ziwa hilo ni karibu meta 750,urefu wake ni karibu  kilometa 1000.





No comments:

Post a Comment