Tuesday, May 10, 2016

Mwenye ulemavu aliyekusudia kuuza figo yake moja

Ni kutokana na ugumu wa maisha

NA KWIRINUS MAPUNDA,NYASA

MWENYE ulemavu wa viungo Vikta Komba(Zambia) ambaye Halmashauri ya Mbinga mkoa wa Ruvuma imeshindwa kumlipa deni lake la sh.milioni 10 anadai anatarajia kuomba kibali cha kuuza moja ya figo zake ili kukabiliana na matatizo  yanayomkabili.
Zambia akionesha nyumba yake ambayo imeanguka

Zambia hivi sasa anaishi katika umasikini mkubwa katika kijiji cha Nkali kata ya Liuli wilayani Nyasa mkoani Ruvuma  baada ya mradi wake wa kuotesha miche kukwama kwa kile ambacho amedai Halmashauri ya wilaya ya Mbinga
kushindwa kumlipa deni lake tangu mwaka 2011.

“Mradi wangu wa kuotesha miche ya miti mbalimbali  hivi sasa umekufa, kwa miaka mingi niliweza kuotesha miche na kuuza katika maeneo mbalimbali ikiwemo ofisi za serikali,shule,taasisi za kidini na watu binafsi,sasa nimebakia kuwa masikini kutokana na Halmshauri kushindwa kunimalizia pesa zangu za mradi’’,alidai Komba.

Uongozi wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma unalalamikiwa kutokana na kudaiwa kushindwa kumlipa mwenye ulemavu wa viungo Zambia zaidi ya sh. milioni 10 za makubaliano ya uoteshaji wa miche 42,000 ya korosho.

Komba alibainisha kuwa baada ya kampuni ya Brink Naturals Enterprises kuchukua eneo lake lenye ekari 12 katika kijiji cha Nkali na kuharibu mazao yake baada ya kuidhinishwa na Halmashauri ya kijiji cha Nkali.

“Niliamua kufungua kesi ya madai mahakamani namba 72 ya mwaka 2007,hata hivyo niliamua kumaliza kesi nje ya mahakama mwaka 2009  baada ya wadaiwa mwenyekiti wa kijiji cha Nkali,mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga na  kampuni ya Brink Natural Enterprises kukubali kutekeleza makubaliano nje ya mahakama yaliofanyika Machi 31,2009 ikiwemo kulipwa kifuta machozi cha shilingi milioni 4.5 ambazo nililipwa”,alisema.  
Zambia akiwa na familia yake

Komba aliyataja makubaliano mengine yaliyofanyika mwaka 2009 kuwa ni Halmashauri ya wilaya ya Mbinga kumpatia kazi ya uoteshaji wa miche ya korosho  zaidi ya 42,000  katika kijiji cha Nkali ambayo Halmashauri ilitakiwa kumlipa zaidi ya shilingi milioni 21 sawa na kila mche wa korosho shilingi 500.

“Mkurugenzi aliniandikia barua ya kukubali kunilipa malipo ya  kuotesha miche ya korosho zaidi 42,000 yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 21 sawa na shilingi 500 kwa kila mche,ingawa baadaye wamenilipa kwa bei ya  shilingi 240 kwa kila mche ambayo ni kinyume cha makubaliano hivyo kulipwa shilingi milioni 10 ambayo ni nusu ya madai yangu’’,alidai Komba.

Hata hivyo Komba ambaye ni mwenye ulemavu wa viungo anadai tangu mwaka 2009  makubaliano ya kulipwa kiasi hicho cha fedha hayajatekelezwa hadi sasa ambapo anaidai Halmashauri ya wilaya ya Mbinga zaidi ya shilingi milioni 10.

Alisema tatizo lake bado halijapatiwa ufumbuzi  hadi sasa na kumsababishia matatizo makubwa ya kiuchumi katika familia yake ikiwemo kushindwa kukamilisha ujenzi wa nyumba yake ambayo imeanza kuanguka na watoto wake wanashindwa kusoma kwa sababu ameshindwa kuwalipia ada.

“Mradi wangu wa kuzalisha miche ya miti zaidi ya 20,000 kila mwaka umekwama ,hivi sasa katika kitalu changu miche inayozalishwa haizidi 1000,ninakabiliwa na madeni mengi,mimi ni mwenye ulemavu,nimeongezewa ulemavu wa kisaikolojia, imefikia mahali malapa tunachangia katika  familia naomba serikali inisaidie’’, alisisitiza.

Komba baba mwenye mke na watoto watano licha ya ulemavu wa viungo alionao ni mkulima na mwanamzingira hodari katika kijiji chake cha Nkali anadai kuwa kutokana na matatizo kuwa mengi anakusudia kuuza moja ya figo katika mwili wake ili apate pesa ambazo zinaweza kutatua matatizo  lukuki yanayomkabili.

“Nimepania kwenda kuomba kibali cha kuuza moja ya figo zangu ili niweze kupata fedha zinakazoniwezesha kutatua matatizo yangu,sina namna nyingine,nyumba inaanguka, watoto wangu watatu wanadaiwa ada ninaishi kwa shida kubwa,’’,alidai Komba.

Barua aliyoandikiwa mwenye ulemavu huyo na  aliyekuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga Shaibu Nnunduma ambaye hivi sasa ni mkurugenzi wa Halmashauri ya  wilaya ya Mafinga imedai kuwa malipo ya shilingi milioni 10  ambayo amelipwa mlalamikaji ndiyo makubaliano halali ambayo wamelipwa waotesha miche ya korosho wote wilayani Mbinga wakati huo hivyo Halmashauri haidaiwi na mlalamikaji Komba.

“Nakuomba Komba endelea kuheshimu makubaliano yetu ya awali yaliofanyika Septemba 12,2011 ofisini kwangu kwenye kikao ,makubaliano yetu yabaki vile vile  usigeuke,unatakiwa kuwa na msimamo ulio thabiti, ’’,imesisitiza  barua ya mkurugenzi huyo.

Mwenyekiti wa chama cha wenye ulemavu  wa viungo mkoa wa Ruvuma  Samwel Mapunda amethibitisha kupata taarifa za  madai ya Zambia katika Halmashauri ya Mbinga  na kwamba chama hicho kimejitahidi kuchukua hatua za kumsaidia mwanachama wao kwa hali na mali ili aweze kupata haki yake yote,hata hivyo alidai kuwa tangu wakati huo hadi sasa amelipwa sehemu tu ya madai yake.





No comments:

Post a Comment