Thursday, May 26, 2016

Mama Janeth Magufuli apongezwa kwa dhamira ya kuwahudumia wazee

Mzee kwanza

Na Albano Midelo

MTANDAO wa Kinga Jamii Tanzania (TSPN) umempongeza  mke wa Rais wa awamu ya tano mama Janeth Magufuli kutokana na dhamira yake ya kuwahudumia wazee wa Tanzania.

Pongezi hizo zimetolewa na katibu mkuu wa TSPN Isikaka Msigwa wakati anazungumza na waandishi wa habari mjini Songea.

Msigwa alisema mtandao wa TSPN unatoa pongezi za dhati kwa mama Janeth Magufuli kwa kuonesha moyo wa upendo mkubwa wa kuwajali wazee wa Tanzania kivitendo ndani ya kipindi kifupi tangu serikali ya awamu ya tano iingie madarakani.


“Ndugu waandishi wa habari, Pongezi hizi  za kipekee kwa Mke wa Rais tunazitoa kwake kutokana na ukweli kuwa, ameonesha moyo  wa pekee wa upendo kwa wazee kwa kutoa msaada mkubwa wa hali na mali katika mikoa mbalimbali ya Tanzania ikiwemo Mkoa wa Dar Es Salaam na Shinyanga’’,alisisitiza.

Alibainisha kuwa upendo huo umekuja wakati muafaka kwani ni wakati ambapo dunia na Tanzania inapigania haki za wazee kwa nguvu zote ikiwemo haki ya kupata tiba, chakula, malazi na huduma nyingine za msingi bila ubaguzi.

Takwimu zinaonesha kuwa Wazee, ndiyo walezi wakubwa wa magonjwa ya muda mrefu, na zaidi ya asilimia 50 ya watoto yatima hapa nchini hulelewa na wazee ambao kimsingi, wao wenyewe wanahitaji kutunzwa kwa kuwa uwezo wao wa kuzalisha mali umepungua na hata wale ambao bado wanajitahidi kuzalisha mali, hawapo kwenye kipaumbele cha miradi mingi inayoendeshwa hapa nchini.

Utafiti unaonesha kuwa vyombo vya kifedha vingi havitoi mikopo  kwa wazee kwa kuhofia kuwa, mzee anaweza kukopa lakini akashindwa kurejesha,  na kwamba wazee hawa  hawana uwezo wa kumudu masharti yanayowekwa na vyombo vya kifedha hata wakiwa tayari kuwakopesha.

Uchunguzi pia umebaini kuwa wazee wengi nchini wana Rasilimali Ardhi ambazo hazina hati miliki. Kutokana na changamoto zote hizo, wazee wengi wanatamani wasingendelea kuishi baada ya kukata tamaa ya maisha.

“Kwa wale wanaomwamini Mungu, watamuunga mkono Mama yetu Janeth Magufuli amechagua fungu lililo jema kwani katika vitabu vya Mungu vinasisitiza kuwaheshimu wazee na malipo kutokana na heshima hiyo, Mungu ameahidi kuanza kumlipa mtu huyo mema kuanzia hapa hapa duniani’’,alisema Msigwa.

Ametoa wito kwa Watanzania kwa ujumla, Taasisi, mashirika, makampuni na Serikali, kuanza kuwapigania wazee kutokana na ukweli kuwa kila amb aye leo ni kijana hana uwezo wa namna yoyote ile kuukwepa Uzee.

Hata hivyo Msigwa alisema ni imani ya TSPN kuona Juhudi ambayo  Mama Janeth Magufuli  ameianza kuonesha mapema kabisa tangu Utawala wa Serikali ya awamu ya tano kuwaunga mkono wazee,na kwamba hiyo ni nia ya dhati ambayo Serikali ya awamu ya tano imedhamiria  kufanya katika kipindi cha miaka mitano  kwa makundi tete wakiwemo wazee.

Alisema Serikali ya awamu ya tano tayari  imeweka Wizara ambayo inashughulikia wazee, pia Serikali  kupitia Wizara ya Afya imeanzisha kauli mbiu ya  ‘’MZEE KWANZA’’ Alikuwa kama wewe utakuwa kama  yeye’

Ametoa wito kwa serikali ya Tanzania kuongeza kasi katika kutunga na kupitisha Sheria ya Wazee mwezi Septemba mwaka huu na kuanza kulipa Pensheni kwa Wazee wote kama ilivyoahidi.

Alisema Ili Tanzania iendelee kubarikiwa na mipango yake kwenda vizuri kama inavyopangwa, Viongozi wengine Serikalini wamuunge mkono Mama Janneth Magufuli kwa kuwaandalia Wazee mazingira mazuri kimaisha waishi kwa amani na furaha katika kipindi ambacho wanaishi ili wasiondoke duniani huku wakiilaumu  Serikali.

Katibu mkuu huyo wa TSPN amewaasa watu binafsi, makampuni, jamii, taasisi nao waunge mkono juhudi hizo za kuboresha maisha ya Wazee wa Tanzania kila mmoja alipo bila kuisubiri Serikali.

Tanzania Social Protection Network (TSPN), ni  muungano wa Mashirika 34  yasiyo ya kiserikali yaliyosajiliwa kisheria kutoka mikoa 26 ya Tanzania bara na Visiwani, yanayojishughulisha na kuwahudumia Wazee, Watu wenye ulemavu wa aina mbalimbali na Watoto waishio katika mazingira hatarishi, mtandao ambao ulioundwa rasmi mwaka 2010.





No comments:

Post a Comment