Sunday, May 15, 2016

Manispaa ya Songea kuwezeshwa bilioni 4.75 za Rais Magufuli



NA KWIRINUS MAPUNDA,SONGEA

Vikundi vya wajasirimali kutoka mitaa 95 ya manispaa ya Songea mkoani Ruvuma vinatarajiwa kuwezeshwa mikopo  ya jumla ya shilingi bilioni 4.95  sawa na kila mtaa kupata shilingi milioni 50.
Abdul Mshaweji meya wa manispaa ya Songea akifungua mafunzo

Afisa habari wa manispaa ya Songea Albano Midelo alisema fedha hizo zinatokana na mpango wa uwezeshaji wananchi milioni 50 kwa kila kijiji au mtaa ambazo zinatolewa na Rais Magufuli kwa mkopo wa masharti nafuu.

Kulingana na afisa habari huyo Baraza la Taifa la uwezeshaji wananchi kiuchumi tayari limetoa
mafunzo ya mpango wa uwezeshaji wananchi milioni 50 kila mtaa ambapo katika manispaa ya Songea vikundi mbalimbali vilipata mafunzo hayo viwemo vyama akiba vya kuweka na kukopa SACCOS na VICOBA.


Akizungumza wakati wa ufunguzi rasmi wa mafunzo hayo,Mstahiki meya wa manispaa ya Songea Abdul Hassan Mshaweji aliviasa vikundi vyote ambavyo vitapata mkopo nafuu wa milioni 50 kuhakikisha kuwa kila mwanakikundi kulipa mkopo huo kwa wakati ili kila mmoja anaweze kunufaika.

“kila mtaa katika manispaa yetu utapata milioni 50 hivyo kwa mitaa yote 95 tunapata shilingi bilioni 4.75,naomba kila mwananchi awe na tabia ya kuweka akiba,kukopa kwa busara,kulipa kwa wakati na kila aliyekopa akumbuke kurudisha pesa hizo kwa kuwa ni mkopo unatakiwa kutumika kwa malengo yaliyokusudiwa’’,alisisitiza Mshaweji.
Wakazi wa manispaa ya Songea wakifuatilia mafunzo

Mstahiki Meya huyo aliwaasa wote watakaopata mkopo huo kuhakikisha kuwa  wanafanya matumizi yatakayowaletea maendeleo kwa kuwa uzoefu unaonesha kuwa watanzania wengi hawana matumizi ya fedha yaliyokusudiwa hivyo aliwaonya fedha hizo sio kwa ajili ya kufanya sherehe bali ni kwa ajili ya maendeleo.

Mshaweji alisema Tanzania inakwenda kwenye uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025 ambapo kipato cha kati ya mtanzania kwa siku kinatarajia kuwa shilingi 67,000 na kwamba uchumi wa kati unakwenda sanjari na  kuanzisha viwanda vidogo na vya kati.

Akitoa mafunzo ya mpango wa  uwezeshaji wananchi milioni 50 za Rais Magufuli kwa kila mtaa na kijiji  kwa mamia ya vikundi vya ujasirimali katika ukumbi wa manispaa ya Songea,mkurugenzi wa mifuko ya uwezeshaji nchini Edwin Chrisant alisema Baraza la Taifa la uwezeshaji wananchi kiuchumi  litasimamia na kuhakikisha kuwa mkopo huo unatolewa bila ubaguzi wa aina yoyote.
Edwin Chrisant mkurugenzi wa mfuko wa uwezeshaji akitoa mafunzo

Chrisant aliwaasa wananchi kuchukua mkopo huo kwa busara na kurejesha kwa utaratibu na kuwakumbusha wale wote waliochukua mkopo wa mabilioni ya Rais mstaafu wa awamu ya nne ambao hawajarejesha mikopo yao wanafahamika na wajiandae kutumbuliwa.

Baraza  la Taifa la uwezeshaji wananchi kiuchumi tayari limetoa mafunzo ya mpango wa uwezeshaji wananchi milioni 50 kwa kila kijiji na mtaa katika Halmashauri tatu za mkoa wa Ruvuma ambazo ni Songea vijijini,Mbinga na Songea manispaa.

Chimbuko la kutolewa mkopo huo wa masharti nafuu katika vijiji na mitaa yote Tanzania linatokana na ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi CCM ya mwaka 2015 ibara ya 57 ambapo CCM iliahidi kuwawezesha wananchi kiuchumi endapo kingefanikiwa kuingia madarakani.

Uwezeshaji wananchi ulioahidiwa katika ilani hiyo ni pamoja na Kutenga shilingi milioni 50 kwa kila kijiji au mtaa kama mfuko wa Mzunguko (Revolving Fund) kwa ajili ya kuvikopesha vikundi vya wajasiriamali kupitia SACCOS na VICOBA,Kusimamia uanzishwaji wa vikundi vya ushirika kama SACCOS na VICOBA na Kuweka mfumo wa kuvitambua na kuvisajili na Kuhakikisha upatikanaji wa mitaji yenye masharti nafuu  bila urasimu wowote.

MWISHO


No comments:

Post a Comment