Na Stephano Mango
Manispaa ya Songea iliyopo mkoani
Ruvuma ni miongoni mwa Halmashauri nchini ambazo zimeweka dhamira ya
kuhakikisha inaweka mikakati ya kuboresha maisha ili kuendana na kasi ya Rais wa
awamu ya tano ya kujenga Tanzania mpya yenye neema.
Afisa habari wa manispaa hiyo Albano
Midelo anasema Baraza la madiwani likiongozwa na mstahiki Meya Abdul Hassani Mshaweji kwa kushirikiana
mkurugenzi wa manispaa hiyo Jenifer Omolo pamoja na wataalam katika idara
zote wameweka maeneo kumi ya vipaumbele
yatakayoiwezesha manispaa hiyo kupaa.
Kwa mujibu wa afisa habari huyo Halmashauri
ya manispaa imeangalia maeneo
ya msingi
katika kuboresha na kuimarisha utoaji wa
huduma kwa kuyapa uzito maeneo hayo ili kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazojitokeza wakati wa
utekelezaji wa majukumu ya msingi ya Halmashauri.
Vipaumbele ambavyo vimepitishwa na Baraza la madiwani la
Halmashauri ya manispaa ya Songea katika bajeti ya mwaka 2016/2017 vimelenga
katika Sekta ya Elimu ambapo Halmashauri imejiwekea malengo katika kuboresha
huduma za jamii hasa katika kuboresha miundombinu ya shule za Msingi na
Sekondari kwa kukamilisha miradi viporo na kujenga miundombinu mipya.
Katika Baraza la madiwani ambalo mbunge wa jimbo la Songea
Leonidas Gama anashiriki kama diwani limeyataja Maeneo yatakayozingatiwa katika
sekta ya elimu kuwa ni pamoja na ujenzi wa madarasa,maabara,mabweni,vyoo,
ukarabati wa madarasa ununuzi wa samani pamoja na mishahara ya watumishi.
Sekta ya Afya ni
miongoni mwa vipaumbele vilivyopitishwa na Baraza hilo Lengo likiwa ni
kuboresha miundombinu ya Vituo vya Afya na Zahanati kwa kuendeleza ujenzi na
upatikanaji wa dawa. Maeneo muhimu ni ujenzi wa zahanati, ukarabati, ujenzi wa
chumba cha upasuaji, samani na ununuzi wa madawa.
| Jenifer Omolo mkurugenzi wa manispaa ya Songea |
Afisa habari huyo amekitaja kipaumbele
kingine ambacho kimewekwa na manispaa ya Songea kuwa ni Sekta ya Maji Lengo likiwa ni kuongeza upatikanaji wa maji
ya kutosha katika maeneo ya pembezoni ya Manispaa kwa kujenga visima vya
maji virefu na vifupi, kuanzisha uvunaji
wa maji ya mvua na kuanzisha mtandao wa maji ya bomba.
Sekta ya ujenzi pia imepewa kipaumbele
katika bajeti ya mwaka 2016/2017 ambapo manispaa ya Songea imejiwekea lengo la
kuboresha miundombinu ya barabara kwa kufanya matengenezo ya mara kwa mara,
maeneo korofi na matengenezo ya kawaida.
Bajeti hiyo pia imeadhimia kujenga
dampo la kisasa, kujenga kituo kuu ya mabasi ya kwenda mikoani, kujenga maeneo
ya maegesho ya malori pikipiki,magari madogo na taksi, kujenga vivuko na
Madaraja, kuweka taa za barabara na ujenzi wa masoko kila kata.
Kipaumbele pia kimewekwa katika Sekta
ya Kilimo,Uvuvi Mifugo na Ushirika Lengo likiwa ni kuendeleza kilimo bora na endelevu kwa
kutumia pembejeo za kisasa kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula
na biashara.
Manispaa ya Songea imedhamiria
kuendeleza kilimo cha umwagiliaji, mafunzo kwa wakulima huduma za ugani na
vituo vya mafunzo na Kuendeleza ufugaji wa ndani hasa Mradi wa kopa ng’ombe lipa
ng’ombe ambao utasaidia kuongeza kipato kwa wananchi.
Sekta ya Mipango Miji, Ardhi na
Maliasili ni miongoni mwa vipaumbele
vilivyopitishwa katika bajeti lengo likiwa ni kuboresha makazi ya wananchi kwa
kuongeza upimaji wa viwanja, na ulipaji wa fidia kuboresha maeneo
yaliyoendelezwa kiholela ambayo yamesababishwa na uhaba wa viwanja
vilivyopimwa.
“Manispaa ya Songea imedhamiria kutoa
hati miliki za ardhi, kuandaa michoro ya Mipangomiji, upandaji wa miti,
utunzaji wa mazingira, utunzaji na uhifadhi wa vyanzo vya maji na utengaji wa
maeneo kwa ajili ya ujasiriamali na kutenga maeneo kwa ajili ya utalii wa ndani
na uwekezaji mkubwa’’,alisema afisa habari huyo.
![]() |
| Abdula Hassan Mshaweji mstahiki Meya wa manispaa ya Songea |
Kwa kuzingatia kuwa kila kitu
kinahitaji Utawala bora,manispaa ya Songea imejiwekea malengo katika kuboresha
mazingira ya kufanyia kazi watumishi katika sekta ya Utawala, Mipango na
Biashara pamoja na utoaji wa huduma kwa Wananchi wa Manispaa.
Ili kuendana na Ulimwengu wa Sayansi na teknolojia,Manispaa ya Songea
imepanga kutoa mafunzo ya muda mfupi na mrefu ya teknohama (ICT) kwa kutumia
mifumo mipya ya mitandao na kutoa mafunzo ya upangaji mipango bajeti, utunzaji
wa takwimu kwa mfumo wa LGMD na IPSAS.
Manispaa hiyo pia inatoa elimu kuhusu
utatuzi wa migogoro sehemu za kazi,utatuzi wa kero wa wananchi, mafunzo ya
sheria mbali mbali zinazohusu mikataba, utumishi elimu ya ujasiriamali na mkataba kwa mteja.
Masuala Mtambuka ambayo yamepewa
kipaumbele katika manispaa ya Songea ni pamoja na kutoa elimu ya kujikinga na
maambukizi ya maradhi mbalimbali kama UKIMWI, Malaria Kifua Kikuu na
kushughulikia masuala ya UKIMWI, magonjwa ambayo hayapewi kipaumbele,Mazingira
na kupambana na Madawa kulevya na rushwa.
Kuhusu kipaumbele cha Uchumi na
Biashara manispaa ya Songea imedhamiri kuanzisha viwanda vya uzalishaji wa
bidhaa na kukuza soko, kuanzisha miradi yenye tija, standi na masoko kuongeza
ukusanyaji wa mapato ya ndani kwa kutumia njia ya kielektroniki, kuongeza
maeneo ya uzalishaji, biashara na utoaji mikopo mbalimbali kwa mtu mmoja mmoja
na vikundi.
Sekta ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na
Watoto pia ni miongoni mwa vipaumbele katika manispaa ya Songea lengo likiwa ni
kutoa elimu ya ujasiliamali na elimu ya kutumia raslimali asilia katika masuala
ya maendeleo,kutoa mafunzo ya matumizi sahihi ya mikopo,ujasiriamali,raslimali
asili kwa vikundi vya Vijana, Wanawake na Wazee kwa maendeleo.
Ili kutekeleza vipaumbele vilivyotajwa na
Halmashauri ya Manispaa ya Songea kwa mwaka wa fedha wa 2016/2017, inakadiria
kutumia zaidi ya shilingi bilioni. 55.
Hata hivyo kwa Mwaka 2016/2017 Manispaa ya Songea inatarajia kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 55 kutoka vyanzo mbali mbali vya mapato. Makisio haya ni sawa na ongezeko la zaidi ya shilingi bilioni 11 sawa na asilimia 21.5 ya lengo la makusanyo kwa mwaka 2015/2016 ambapo lengo lilikuwa ni kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 43.
mwisho


No comments:
Post a Comment