Thursday, July 21, 2016

Ondoeni kero kwa wananchi



Kila mtumishi wa umma awajibike
Mkuu wa mkoa wa Ruvuma  Dk.Binilith Mahenge amewaagiza  watumishi wa umma mkoani humo kuwajibika kwa wananchi na kuwaondolea kero mbalimbali zinazowakabili.

Dk.Mahenge alitoa agizo hilo wakati anazungumza na wakuu wa idara wa manispaa na Taasisi za umma kwenye kikao na viongozi wa wazee na wafanyabiashara kilichofanyika kwenye ukumbi wa manispaa ya Songea.


Ameagiza watumishi wote wa umma kufanya jitihada za dhati za kuwaondolea kero wananchi katika maeneo yao na kusisitiza kuwa watendaji wasiwe chanzo cha kero
katika maeneo ambayo wanayaongoza.

“Nataka kuona matokeo mazuri kwa kila kazi inayofanywa na mtumishi wa serikali,tabia ya kuorodhesha kero,changamoto,na matatizo siyo suluhisho la utendaji kazi.Lugha za njoo kesho,tupo kwenye mchakato sasa zifikie mwisho kwa watumishi wanaowahudumia wananchi’’,alisisitiza.

Dk.Mahenge amewaagiza viongozi wa Taasisi  mbalimbali za umma kufanyakazi kwa waledi wa taaluma zao ili kutoa huduma kwa wananchi katika kiwango cha ubora unaohitajika.

Hata hivyo mkuu huyo wa mkoa amewapongeza wananchi na wadau wote wa maendeleo kutokana na kuunga mkono jitihada mbalimbali za serikali ya awamu ya tano ambazo zimesababisha kufikia malengo ambayo yameanza kuonekana.

Kwa upande wake mbunge wa Songea mjini Leonidas Gama amewaasa wakazi wa manispaa ya Songea kumpa ushirikiano mkubwa mkuu wa mkoa mpya ambapo amesema mkoa umempata mkuu wa mkoa mchapakazi ambaye anaweza kuupaisha mkoa huo kulingana na malengo ya serikali ya awamu ya tano.

Gama amewaasa wakazi wa manispaa ya Songea na watumishi wa umma sasa kila mmoja achape kazi badala ya kujiingiza kwenye migogoro ya wanasiasa hivyo kuzorotesha maendeleo endelevu.

Rais Dk.John Magufuli amemteua Dk.Binilith Mahenge  kuwa mkuu mpya wa mkoa wa Ruvuma ambaye amechukua nafasi ya aliyekuwa mkuu wa mkoa huo Said Mwambungu ambaye amehamishiwa ofisi ya waziri mkuu.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment