St.Vinsenti shule ya msingi ya elimu
maalum ya wenye ulemavu wa kusikia iliyowahi kupewa cheti cha ubora wa shule
Tanzania mwaka 2000 kutoka wizara ya elimu
kutokana na kufaulisha karibu kila mwaka darasa zima.
Shule ya mtakatifu Vincenti
inayomilikiwa na watawa wa kanisa katoliki imeanzishwa katika kata ya Ruhuwiko manispaa ya Songea
mkoani Ruvuma.
Shule hiyo imejengwa katika viwanja
ambavyo vilitumiwa na aliyekuwa kiongozi mkuu wa kanisa katoliki Duniani mwaka
1990 katika adhimisho la misa takatifu.Hayati
papa yohanne Paulo wa pili Septemba 1990
alifanya ziara ya kutembelea nchi kadhaa barani Afrika ikiwemo Tanzania
.
.
Miongoni mwa mikoa ambayo kiongozi
huyo wa ngazi ya juu wa kanisa katoliki Duniani aliweza kuitembelea na kufanya
adhimisho la misa takatifu ni eneo la Ruhuwiko mjini Songea mkoa wa Ruvuma.
Kutokana na umuhimu wa ujio wa papa
Yohanne Paulo wa pili kanisa katoliki jimbo kuu la Songea liliona umuhimu wa
eneo hilo kuweka kumbukumbu ya ujio wa Papa ndiyo maana ikapendekezwa kujengwa
shule ya bweni ya wenye ulemavu wa kusikia yaani viziwi inayoitwa St.Vincenti.
Mkuu wa shule hiyo Sr.Anna Mgaya
anasema St.Vincent ni miongoni mwa shule ambazo zinatoa mchango mkubwa kwa
wenye ulemavu hapa nchini inahudumia watoto wenye ulemavu katika kundi la
viziwi.
Anabainisha kuwa shule hiyo
inawahudumia wenye ulemavu viziwi kutoka mikoa mbalimbali nchini ikiwemo
Ruvuma, Njombe, Iringa, Mbeya,Dar es salaam,Rukwa na Mtwara.
Kwa mujibu wa Sr.Mgaya shule ya St.Vinsenti ilianzishwa
mwaka 1984 na kanisa katoliki jimbo kuu la Songea baada ya kufanyika
makubaliano kati ya kanisa na serikali.
“Makubaliano hayo yalifanyika baada ya
kufanyika utafiti na kugundulika kuwa wapo watoto wengi viziwi katika ukanda ya
kusini ambao wanakosa nafasi ya shule baada ya ukanda mzima wa kusini kutokuwepo
kwa shule ya walemavu viziwi”,alisema.
Shule hiyo ilipata usajili Januari
15,1989 na kupewa namba RV/01/02/033 na ilifunguliwa rasmi na waziri mkuu mstaafu hayati Rashid Mfaume Kawawa Februari 2,1992 ambaye
siku ya ufunguzi alipanda mti wa kumbukumbu ambao bado upo hadi leo.
Kulingana na Sr.Mgaya shule hiyo ina uwezo wa kupokea wanafunzi wasiozidi 200
tu na kwamba kutokana na hali hiyo Kila mwaka watoto wanye ulemavu viziwi wengi
wanakosa nafasi ya kujiunga katika shule hiyo kutokana na shule kukosa uwezo wa
kuchukua wanafunzi wengi zaidi ya hao.
“kutokana na changamoto zilizopo idadi
ya wanafunzi waliopo hivi sasa katika shule yetu ni 140 ambao wanasoma
kuanzia shule ya awali hadi darasa la
saba”alisema na kuongeza kuwa shule hiyo ina kitengo cha ufundi katika fani za
useremala,ushonaji,,upimaji na utengenezaji wa shime sikio kwa ajili ya viziwi.
Ameyataja baadhi ya mafanikio yaliopatikana tangu
kuanzishwa kwa shule hiyo kuwa ni shule kujitosheleza katika majengo na
samani,vifaa vya kujifunzia na kufundishia mazingira mazuri ya
kujifunzia,kufundishia na nyumba za walimu zinazokidhi mahitaji ya walimu.
Sr.Mgaya amesema shule hiyo inafanya
vizuri kitaaluma ambapo kila mwaka karibu wanafunzi wote wanachaguliwa
kuendelea na masomo ya sekondari katika shule zinazochukua wanafunzi wenye
ulemavu zikiwemo za Njombe na Iringa.
“Kwa mfano matokeo ya mwaka juzi ya darasa la
saba yanaonesha kuwa wanafunzi waliofanya mtihani walikuwa 19,wanafunzi wote
walifaulu, shule yetu ngazi ya wilaya ilishika nafasi ya saba kati ya shule
75,kimkoa ilikamata nafasi ya 78 kati ya shule 729 na kitaifa shule ilikuwa ya
1854 kati ya shule 15,867’’,alisema.
Shule hiyo ina kitengo cha ufundi ambacho kinatoa mafunzo ya awali katika fani za
useremala na ushonaji na kufanya mitihani ya VETA na kupewa vyeti vya ufundi kila mwaka.
Pia Shule hiyo imeanzisha darasa la
kompyuta ili kuendana na ulimwengu wa sayansi na teknolojia kutokana na ukweli
kuwa wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia wana uwezo mkubwa katika masomo ya
vitendo hivyo wanaweza kufanya vizuri katika
somo hilo.
Hata hivyo shule kwa ajili ya watu
wenye ulemavu hapa nchini bado ni changamoto kubwa kutokana na ukweli kuwa hadi
sasa kuna shule chache tena nyingi zinamilikiwa na taasisi binafsi na mashirika
ya dini licha ya kwamba idadi ya watu wenye ulemavu inaendelea kuongezeka.
Kwa mfano Halmashauri ya manispaa ya
Songea ina shule 10 zenye wanafunzi
wenye mahitaji maalum kati ya hizo shule moja ni ya sekondari ambayo ni shule ya wavulana
Songea na vitengo nane katika shule
za msing za serikali na shule moja ya
mtakatifu Vincenti inayomilikiwa na kanisa katoliki.
Kaimu afisa elimu wa manispaa ya
Songea Sunday Wahyungi amezitaja shule za msingi zenye vitengo vya elimu maalum
kuwa ni Luhira, Chandarua, Mitawa, Mahiro, Ndilimalitembo, Subira,Mfaranyaki na
Chemchem.
kulingana na takwimu za idara ya elimu
ya manispaa hiyo hadi kufikia mwezi Mei,2016 katika shule hizo kuna jumla ya
wanafunzi 328 wenye ulemavu wa aina mbalimbali ukiwemo viziwi, ngozi,
akili,viungo na wanafunzi wenye ulemavu zaidi ya mmoja.
Takwimu za wenye ulemavu katika mkoa
wa Ruvuma kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 inaonesha
kuwa kuna watu 523 wenye
ualbino,wasioona zaidi ya 20,000,viziwi zaidi ya 12,000,wenye ulemavu wa viungo
zaidi ya 15,000,,wenye ulemavu wa akiri 14,000 na wenye aina nyingine za
ulemavu karibu 5000.
Tanzania imekuwa na ongezeko kubwa
la watu wenye ulemavu wa aina mbalimbali ambao wanahitaji mahitaji
maalum ya elimu,miundombinu pamoja na mahitaji mengine.
Kulingana na sensa hiyo Tanzania ina
zaidi ya watu 16,000 wenye ualbino,wasioona zaidi ya 848,000,viziwi zaidi ya
425,000,ulemavu wa viungo zaidi ya 525,000,ulemavu wa akiri zaidi ya 400,000,
na karibu 100,000 wana ulemavu wa aina nyingine.
Mwandishi
wa makala haya ni Albano Midelo ambaye amebobea katika masuala ya
elimu,mazingira,madini,gesi na mafuta anapatikana kwa simu 0784765917,baruapepe
albano.midelo@songeamc.go.tz

No comments:
Post a Comment