MRATIBU wa UKIMWI na
tiba katika manispaa ya Songea mkoani Ruvuma Felista Kibena amesema zaidi ya
watu 21,000 katika manispaa ya hiyo wanaishi na virusi vya UKIMWI.
![]() |
| Felista Kibena |
Ofisa habari wa
manispaa hiyo Albano Midelo amesema,Kibena alitoa takwimu hizo wakati
anatoa mada ya ukweli kuhusu virusi vya
UKIMWI na ugonjwa wa UKIMWI kwa
watumishi wa manispaa hiyo mafunzo ambayo yamefanyika kwa siku mbili kwenye
ukumbi wa manispaa ya Songea.
Kwa mujibu wa Kibena
kati ya watu wenye virusi,watu zaidi ya 10,000 ndiyo wanaugua ugonjwa wa UKIMWI
na kutumia dawa za kurefusha maisha za ARV na kwamba maambukizi ya virusi vya
UKIMWI katika manispaa ya Songea ni asilimia nne.
Hata hivyo amesema
mkoa wa Ruvuma unashika nafasi ya tano kitaifa ukiwa na maambukizi ya asilimia
saba ambapo mkoa wa Njombe ndiyo unaongoza kitaifa ukiwa na asilimia 14.5,nafasi ya pili inashika na mkoa
wa
Iringa,ikifuatiwa na mkoa wa Mbeya kwa nafasi ya tatu na mkoa wa Rukwa ukiwa
nafasi ya tano.
“Kiwango cha
maambukizi katika mkoa wa Ruvuma kinapanda kwa kasi awali kiwango cha
maambukizi kilikuwa ni asilimia tano lakini sasa ni asilimia saba,tumevuka
kiwango cha kitaifa ambacho ni asilimia tano’’,alisema.
Hata hivyo amesema
maambukizo makubwa ya virusi vya UKIMWI hivi sasa yanachangiwa na makundi
maalum ambayo aliyataja kuwa ni watu wanaofanya ngono kinyume cha maumbile,watu
wanaofanya biashara ya ngono,wafungwa na watumiaji wa madawa ya kulevya kwa
njia ya kujidunga sindano au kubwia.
Kibena alisema
maambukizo ya virusi katika makundi maalum yamefikia asilimia 36 ambapo kila
watu 100 watu 36 wana virusi vya UKIMWI ukilinganisha na kiwango cha kitaifa
cha asilimia tano ambayo ni sawa na kila watu 100 watano wana virusi.
Amezitaja kata ambazo
zinaongoza kwa maambukizo ya virusi vya UKIMWI katika manispaa ya Songea kuwa
ni Bombambili, Mateka,Ruvuma na Lilambo.
Takwimu za kitaifa
zinaonesha kuwa hadi kufikia mwaka 2013 hapa nchini watu milioni moja na nusu
walikuwa wanaishi na virusi ambapo kwa mwaka 2014 pekee takwimu zinaonesha kuwa
katika Tanzania watu 74,000 wameambukizwa virusi na zaidi ya watu laki tano
walikuwa wanatumia dawa za ARV ambapo hadi sasa watu zaidi ya laki sita
wanatumia ARV.
Kwa mujibu wa takwimu
za shirika la Afya Duniani watu milioni
35 wanaishi na virusi vya UKIMWI hadi kufikia mwaka 2013 kati yao watu milioni 24 sawa na asilimia 71 walitoka
nchi za kusini mwa jangwa la Sahara ambapo watu milioni moja na nusu wamekufa
hadi kufikia mwaka 2013 na watu milioni 12 wanatumia dawa za ARV.
MWISHO

No comments:
Post a Comment